
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan leo Mei 19, 2026 ameondoka nchini kuelekea Kigali, Rwanda kushiriki mkutano wa uvumbuzi wa nishati ya nyuklia barani Afrika (Neisa 2026) hatua inayotarajiwa kufungua zaidi ushiriki wa Tanzania katika ajenda ya matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, mkutano huo unawakutanisha viongozi wa Serikali, wataalamu, wawekezaji, wadhibiti pamoja na wadau wa sekta hiyo kujadili nafasi ya nishati ya nyuklia katika kuimarisha usalama wa nishati, maendeleo ya viwanda na endelevu barani Afrika.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo unaipa nafasi nchi kushiriki katika ajenda ya Afrika kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali ikiwemo nishati, afya, kilimo, viwanda na utafiti.
Aidha, mkutano huo unatarajiwa kujadili namna nchi za Afrika zinavyoweza kutumia teknolojia ya nyuklia kama nyenzo ya kuongeza uzalishaji wa nishati na kuchochea ukuaji wa uchumi, huku zikizingatia usalama na viwango vya kimataifa.
