Karne nyingi baada ya kumalizika biashara ya utumwa ya kuvuka Atlantiki, moja ya masuala nyeti zaidi ya kihistoria yameibuka tena katika mji mkuu wa Ghana, Accra, ambapo Mkutano wa Dunia kuhusu Fidia ya Utumwa na Haki ya Kihistoria ulihitimishwa jana, huku Afrika ikitaka kuwepo mfumo wa vitendo wa kufidia jamii ambazo bado zinateseka kutokana na athari mbaya za enzi hizo.

Kwa siku tatu, washiriki katika mkutano huo walijadili athari mbaya za miongo kadhaa ya utumwa na ukoloni, wakitaka kufanyike tathmini ya uharibifu uliosababishwa na kipindi hicho, na kuchukuliwa hatua za kutambua uhalifu wa kihistoria hadi kuanzisha mifumo iliyo wazi ya kufikia kile kilichotajwa kama haki ya fidia.

Miongoni mwa wanaoongoza kampeni hiyo ni Rais wa Ghana, John Dramani Mahama, ambaye amesema kwamba hatua inayofuata inapaswa kuwa zaidi ya utambuzi wa kinembo tu, kuelekea kwenye kuanzisha muundo ulio wazi wa haki ya fidia ambayo itahakikisha kwamba maamuzi ya kimataifa katika kadhia hii yanatekelezwa kivitendo.

Rais wa Gaza amesisitiza kwamba kinachohitajika ni kudumisha kasi inayotokana na azimio la hivi karibuni la Umoja wa Mataifa, na kufanya kazi ya kutekeleza kivitendo utambuzi wa kimataifa na kuwa hatua halisi zinazoshughulikia athari za zama zilizopita.

Hatua hiyo ya Kiafrika ya kudai fidia ya kipindi cha utumwa ulioanzishwa na wazungu barani humo inakuja baada ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kupitisha azimio Machi mwaka huu kwa wingi wa kura 123, ambalo lilitambua biashara ya utumwa ya kuvuka Bahari ya Atlantiki kuwa mojawapo ya uhalifu mbaya zaidi uliofanywa dhidi ya ubinadamu, na kutoa wito wa kuomba msamaha rasmi na kutolewa fidia kwa jamii zilizoathiriwa na zama hizo.

Makadirio ya kihistoria yanaonyesha kwamba takriban Waafrika milioni 12.5 walitekwa nyara na kusafirishwa kuvuka Bahari ya Atlantiki wakati wa biashara ya watumwa, ambapo zaidi ya Waafrika milioni 10 walinusurika na kuuzwa katika makoloni ya Amerika na Karibiani kama watumwa.

Marekani ilikuwa mojawapo ya maeneo maarufu zaidi kwa watumwa kutoka Afrika, kwani makadirio yanaonyesha kwamba takriban Waafrika 400,000 walipelekwa huko tangu 1619, kabla ya idadi hiyo kuongezeka kadiri utumwa ulivyoendelea na kufikia takriban watumwa milioni nne kufikia 1860.

Licha ya kupita karne nyingi tangu enzi hizo, suala la Waafrika kulipwa fidia bado lipo hai, hasa nchini Marekani, ambapo makundi mengi ya Wamarekani Weusi yanataka suala hilo lijadiliwe tena katika kila msimu wa uchaguzi wa rais, kwani linahusishwa na athari mbaya za kijamii na kiuchumi ambazo bado zinaokana waziwazi.

Wanaodai fidia hiyo wanasema kwamba utumwa haukuwa tukio la kihistoria la kupita tu lililokomeshwa kisheria, bali uliacha mapengo ya kiuchumi na kijamii ambayo yanaendelea katika vizazi vingi, na kwamba kushughulikia athari hizo kunahitaji hatua zinazozidi kuomba msamaha hadi kuchukua hatua za vitendo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *