Dar es Salaam. Tanzania inaendelea kusomesha maelfu ya walimu watakaokuja kufundisha baadaye kila mwaka, lakini utafiti mpya unaonyesha kuwa wengi wao wanaingia darasani wakati wa mafunzo kwa vitendo, wakiwa hawajajiandaa vizuri, bila msaada wa kutosha na wakiwa wameelemewa, hali inayozua wasiwasi juu ya ubora wa elimu nchini.

​Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Dodoma umebainisha changamoto zinazowakabili walimu tarajali wakati wa mafunzo kwa vitendo, ikiwa ni pamoja na uoga wa kumudu darasa, ukosefu wa usimamizi wa karibu kutoka kwa walimu wakuu, kutengwa kitaaluma, na uhaba mkubwa wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia shuleni.

​Utafiti huo uitwao:  ‘Enhancing Teacher Training: A SWOT Perspective on Practicum Experiences in Tanzanian Higher Education’, ulifanywa na mtafiti Mariam John Nyang’anyi na kuchapishwa katika jarida la kitaaluma la Journal of Educational Management and Policy Issues la mwaka 2025.

​Kulingana na mahojiano, uchunguzi wa dondoo za darasani, na uchambuzi wa nyaraka uliowahusisha walimu tarajali 12 waliopangwa katika shule za sekondari mkoani Morogoro, utafiti huo unatoa picha ya kina kuhusu uzoefu wa mafunzo kwa vitendo nchini.

Katika msingi wa matokeo hayo, mtafiti anabainisha kuwa kuboresha ubora wa elimu nchini,  kuna uhusiano wa karibu sana na kuimarisha maandalizi ya walimu, hasa kipengele cha mafunzo kwa vitendo ambapo walimu tarajali wanakutana na mazingira halisi ya darasa kwa mara ya kwanza.

​“Mafunzo kwa vitendo ni muhimu kwa ajili ya kuunganisha nadharia na vitendo,” unabainisha utafiti huo na kuongeza kuwa yanawasaidia walimu tarajali kukuza ujuzi wa kufundisha kupitia uwasilishaji wa masomo, upangaji, na kupokea maoni kutoka kwa wasimamizi wao.

Changamoto zilizopo

​Hata hivyo, matokeo ya utafiti huo yanaonyesha kuwa walimu tarajali wengi hawajaandaliwa kikamilifu kukabiliana na changamoto za kihisia na kisaikolojia zinazoambatana na ufundishaji.

​Changamoto kubwa iliyobainishwa ni ile ambayo mtafiti aliita mwelekeo wa kujitilia shaka, huku walimu tarajali wakiripoti matatizo katika kuzungumza mbele ya watu, kudhibiti nidhamu ya darasa, na kumudu madarasa yenye wanafunzi wengi mno.

​“Nakuwa na aibu kubwa ninapozungumza kwa sauti kubwa mbele ya makundi ya watu, hali inayosababisha kutojiamini na kujihisi shakani mara kwa mara katika mazingira ya kijamii ya ufundishaji,” alisema mwalimu tarajali mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Alex.

​Mwalimu tarajali mwingine, Grace, alikiri kuwa bado anaona ni vigumu kufuatilia nidhamu ya wanafunzi, licha ya kuwa tayari amekamilisha vipindi viwili vya mafunzo kwa vitendo.

​“Licha ya kumaliza mafunzo mawili kwa vitendo, nasita kufuatilia nidhamu ya wanafunzi kwa sababu ya kutokuwa na uhakika wa matokeo yake,” alisema Grace.

​Hali hii inaibua maswali mazito kuhusu kama taasisi za mafunzo ya ualimu nchini zinawaandaa wanafunzi ipasavyo zaidi ya nadharia za kitaaluma, ili kujumuisha utayari wa kihisia na kujiamini wanapokuwa darasani.

​Kulingana na utafiti huo, changamoto kama hizo zinaweza kudhoofisha ufanisi wa ufundishaji na hatimaye kuathiri matokeo ya wanafunzi katika mitihani yao.

​Mwalimu tarajali kutoka Dar es Salaam, ambaye alimaliza mafunzo yake ya vitendo mkoani Pwani na kuomba jina lake lihifadhiwe, aliliambia gazeti hili kuwa ukosefu wa mwongozo shuleni bado ni changamoto sugu.

​“Unafika shuleni ukiwa na shauku kubwa, lakini wakati mwingine hakuna mtu anayekuongoza vizuri. Baadhi ya walimu wanatuchukulia kama mzigo wa kazi ya ziada badala ya kutuona kama wafanyakazi wenzao wa baadaye,” alisema mwalimu huyo huku akisisitiza kuwa maoni kuhusu ufundishaji wao kutoka kwa walimu wazoefu, yalikuwa machache sana.

​Utafiti huo pia uligundua kuwa usimamizi mbovu na kutengwa kitaaluma na walimu wenye uzoefu ni vikwazo vikubwa vinavyoathiri maendeleo ya walimu tarajali.

​“Kutengwa nilikoshuhudia kutoka kwa walimu waliopo kazini kunapunguza umakini wangu katika juhudi za ufundishaji,” alisema mwalimu mwingine tarajali aliyetambuliwa kama Hellen.

​Watafiti pia walitaja miundombinu mibovu na uhaba wa vifaa vya kujifunzia kama vikwazo vikuu ambapo uchunguzi ulionyesha uwepo wa madarasa yenye wanafunzi wengi kupita kiasi, fursa ndogo ya kuingia maabara, na rasilimali duni za kufundishia, hali inayowalazimu walimu tarajali kutegemea mbinu mbadala za kubahatisha.

​Licha ya changamoto hizo, utafiti huo ulibainisha matokeo kadhaa chanya kutokana na uzoefu huo, ambapo walimu tarajali wengi waliripoti maendeleo katika upangaji wa masomo, ujuzi wa mawasiliano, mwingiliano wa darasani, na ugunduzi.

​Baadhi walisema uzoefu huo uliwasaidia kuunganisha ujuzi wa nadharia na vitendo halisi vya darasani, wakati wengine waliona mabadiliko chanya katika uwezo wa kuhimili changamoto na kwenda na wakati.

​Kutokana na hali hiyo, utafiti unapendekeza kuwepo kwa mageuzi yanayojumuisha ushirikiano wa karibu zaidi kati ya vyuo vikuu na shule, mifumo thabiti na rasmi ya usimamizi, mafunzo ya ustahimilivu wa kihisia, maandalizi bora ya jinsi ya kumudu darasa, pamoja na tathmini nzuri ya shule wanakopelekwa walimu hao.

​Pia unatoa wito wa kuongezwa kwa uwekezaji katika rasilimali za shule, hasa katika maeneo ya vijijini ambako mazingira ya kufundishia bado ni magumu zaidi.

​Utafiti huo unatanabahisha kuwa mafunzo kwa vitendo yanaweza kuwa daraja muhimu kuelekea kwenye taaluma ya ualimu, au yakawa uzoefu wa kukatisha tamaa unaowafukuza walimu vijana mbali na taaluma hiyo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *