Dar es Salaam. Kadiri siku zinavyozidi kwenda ndipo matumizi ya vifaa vya kisasa vyenye teknolojia ya hali ya juu vinazidi kushika kasi kama kifaa hiki kipya kinachotumia akili unde (AI) kiitwacho ‘Fitbit Air’ kilichotengenezwa kwaajili ya kufuatilia afya yako.

Kampuni ya Google kupitia kitengo chake cha vifaa vya afya imezindua kifaa hiki cha kuvaa mkononi chenye lengo la kusaidia watumiaji kufuatilia afya zao kwa urahisi zaidi. 

Kifaa hicho kinatajwa kuwa chepesi, rahisi kuvaa na kinatumia AI kutoa taarifa mbalimbali huku kwa mujibu wa Google, kina uwezo wa kufuatilia mapigo ya moyo, kiwango cha oksijeni mwilini, usingizi pamoja na mwenendo wa mazoezi ya mtumiaji kwa saa 24. 

Tofauti na saa nyingi za kisasa zenye skrini kubwa, Fitbit Air imeundwa kwa mfumo mdogo zaidi unaotegemea programu maalum ya simu kutoa taarifa na ushauri kupitia AI.

Wataalamu wa teknolojia wanaeleza kuwa hatua hiyo inaonyesha namna kampuni mbalimbali zinavyoanza kuelekeza nguvu katika vifaa vidogo vinavyoweza kufanya kazi nyingi bila kutumia nguvu kubwa ya betri au gharama kubwa. 

Uzuri wa kifaa hiko kinapunguza mzigo wa kubeba simu yenye programu za ufatiliaji wa afya muda wote na badala yake Fitbit Air inachukua nafasi. 

Kampuni ya Google imezindua rasmi kifaa chake kipya cha kisasa cha kufuatilia afya kinachojulikana kama *Fitbit Air*, hatua inayotajwa kuwa sehemu ya ushindani mkubwa wa teknolojia ya vifaa vinavyovaliwa mwilini duniani.

Katika taarifa iliyotolewa Mei 7, 2026 kupitia blogu rasmi ya kampuni hiyo, Google imesema kifaa hicho kipya kimetengenezwa kwa mfumo usio na skrini, kikiwa chepesi zaidi na rahisi kuvaliwa muda wote huku kikitoa taarifa za kina kuhusu afya ya mtumiaji.

Mkuu wa Bidhaa wa Google Health, Andy Abramson, alisema watu wengi bado huona vifaa vya kisasa vya kuvaa mwilini kuwa vikubwa, vigumu kutumia au vyenye gharama kubwa, jambo lililoisukuma kampuni hiyo kuja na Fitbit Air.

“Fitbit Air ni rahisi, nafuu na linaweza kuvaliwa saa zote bila usumbufu. Limeundwa kusaidia watu wengi zaidi kupata taarifa binafsi za afya zao kupitia Google Health Coach,” alisema Abramson.

Google imesema kifaa hicho kina uwezo wa kudumu na chaji kwa hadi wiki moja bila kuchajiwa tena. Aidha, mtumiaji anaweza kupata matumizi ya siku nzima kwa dakika tano pekee za kuchaji kifaa hicho.

Katika upande wa mazoezi, Fitbit Air inaweza kutambua moja kwa moja baadhi ya shughuli za mwili kama kukimbia, kutembea au mazoezi ya kawaida bila mtumiaji kuanzisha mfumo mwenyewe. Kampuni hiyo imesema teknolojia hiyo huendelea kujifunza tabia za mtumiaji kadri anavyoendelea kutumia kifaa hicho.

Mbali na teknolojia ya afya, Google pia imeweka mkazo kwenye muonekano wa kifaa hicho kwa kuzindua aina mbalimbali za mikanda ya kuvaa ikiwemo mikanda ya mazoezi, matumizi ya kawaida pamoja na matoleo ya kisasa zaidi ya mitindo.

Kifaa hicho kinatarajiwa kuuzwa kwa dola 99.99 za Marekani sawa na karibu na Sh260,000 huku Google ikisema Fitbit Air itapatikana kwa watumiaji wa simu za Android pamoja na iPhone.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *