Dar es Salaam. Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Abdel Fattah El-Sisi, anatarajiwa kuwasili nchini kesho Julai 18, 2026 kwa ziara rasmi ya kitaifa kufuatia mwaliko wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Katika ziara hiyo, Rais El-Sisi atapokewa rasmi Ikulu, Dar es Salaam, kabla ya kufanya mazungumzo ya pande mbili na mwenyeji wake, Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Julai 17, 2026 na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, mazungumzo hayo yanatarajiwa kujikita katika kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na Misri katika sekta mbalimbali za kiuchumi, pamoja na kujadili fursa mpya za ushirikiano katika maeneo ya kimkakati yenye manufaa kwa mataifa hayo mawili.

Viongozi hao pia wanatarajiwa kuzungumza na waandishi wa habari na kuelezea makubaliano na maazimio yatakayofikiwa katika mazungumzo yao, pamoja na msimamo wao wa kuendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Misri.

Mbali na mazungumzo ya viongozi hao, Rais Samia na Rais El-Sisi watazindua Jukwaa la Biashara la Tanzania na Misri litakalowakutanisha wawekezaji, wafanyabiashara, wawakilishi wa sekta binafsi na viongozi wa Serikali kutoka nchi hizo mbili.

Jukwaa hilo linatarajiwa kujadili fursa mpya za uwekezaji, kukuza biashara na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kwa lengo la kuongeza ustawi wa wananchi wa Tanzania na Misri.

Ziara ya Rais El-Sisi ni ishara ya kuendelea kuimarika kwa uhusiano wa kihistoria na ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Misri, huku ikitarajiwa kufungua fursa mpya za maendeleo na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya mataifa hayo mawili.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *