
Wanazuoni wa Bahrain wametoa onyo kuhusu kuendelea ukiukwaji wa haki za binadamu nchini humo, wakisema hali hiyo inazidi kuzorota na kuhatarisha haki za msingi za wananchi.
Katika taarifa yao, wanazuoni hao walieleza wasiwasi wao kuhusu hatua za kukandamiza uhuru wa kujieleza, uhuru wa kuabudu na haki nyingine za kiraia, huku wakitoa wito kwa mamlaka husika kuheshimu sheria na viwango vya kimataifa vya haki za binadamu.
Aidha, wamesisitiza umuhimu wa kulinda utu wa binadamu, kuzingatia haki za wananchi wote bila ubaguzi, na kutafuta suluhu kupitia mazungumzo na maridhiano ya kitaifa ili kudumisha amani na utulivu nchini Bahrain.
Kwa mujibu wa tovuti ya habari ya Vijana wa Mapinduzi ya Februari 14 ya Bahrain, kundi la wanazuoni mashuhuri wa nchi hiyo limetoa taarifa likilaani kile walichokiita vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu vinavyotekelezwa na utawala wa Aal Khalifa kupitia kuwafuatilia, kuwakamata na kuwafikisha mahakamani wanazuoni wa dini, wahubiri na waenezaji wa madhehebu ya Kishia.
Wanazuoni hao wamesema hali ya sasa inayowakabili Waislamu wa Kishia nchini Bahrain imefikia kiwango cha kutishia uwepo wao, wakieleza kuwa hatua hizo zinahatarisha uhuru wa dini, haki za kiraia na mshikamano wa kijamii nchini humo.
Jumuiya ya Kitaifa ya Kiislamu ya Al-Wifaq ya Bahrain nayo pia imesisitiza kuwa, viongozi wa Bahrain wanatekeleza kwa makusudi siasa na sera za maudhi na manyanyaso ya kidini nchini humo na kwamba hatua kali hizo zimeshtadi baada ya vuguvugu la mapinduzi ya Februari 14, 2011.