
Ndege elfu moja zisizo na rubani za kimkakati zimejiunga na vikosi vinne vya jeshi kwa amri ya Meja Jenerali Amir Hatami, Kamanda Mkuu wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Ndege hizo 1,000 zisizo na rubani za kimkakati, ambazo zimejiunga na vikosi vya mapigano vya jeshi kwa amri ya Meja Jenerali Amir Hatami, zimetengenezwa na wataalamu wa jeshi kwa ushirikiano na Wizara ya Ulinzi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kulingana na vitisho vipya na uzoefu wa Vita vya Siku 12. Ndege hizo zimeundwa katika kategoria za uharibifu, mashambulizi, upelelezi na vita vya kielektroniki ili kuharibu shabaha maalumu thabiti na za kuhamahama baharini, angani na nchi kavu.
Baada ya kutoa agizo la kuunganishwa ndege zisizo na vikosi vya jeshi, Meja Jenerali Amir Hatami, Kamanda Mkuu wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, amesema: “Sambamba na vitisho vilivyo mbele, miongoni mwa ajenda za jeshi ni kudumisha na kuimarisha faida za kimkakati kwa mapigano ya haraka na kutoa majibu makali kwa uvamizi na uchokozi wa aina yoyote.”
Wakati huo huo, Ali Shamkhani, mwakilishi wa Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu katika Baraza la Ulinzi la Iran, ameandika kwenye akaunti yake kwenye mtandao wa kijamii wa X kwamba: “Hatua yoyote ya kijeshi itakayofanywa na Marekani, kutoka chanzo chochote na katika ngazi yoyote, itatambuliwa kuwa ni mwanzo wa vita, na majibu yake yatakuwa ya haraka, ya kina, na yasiyotarajiwa.”