BAADA ya beki wa kushoto wa Bigman FC, Adeyum Saleh kukosekana kwa wiki mbili kutokana na majeraha ya kifundo cha mguu, nyota huyo ameanza mazoezi rasmi na kikosi hicho, huku akiahidi kuendelea kupambana zaidi katika mechi zilizobakia.

Akizungumza na Mwanaspoti, Adeyum amesema baada ya kukosa takriban mechi mbili za timu hiyo kwa sasa hali ya afya yake imezidi kuimarika tofauti na mwanzoni, ingawa jambo lililobakia ni kwa benchi la ufundi la timu hiyo kuamua kumtumia.

“Kwa sasa niko vizuri na nimeanza mazoezi binafsi na kujumuika na wachezaji wenzangu, hayakuwa majeraha makubwa sana ndiyo maana nimetumia muda mfupi kurudi haraka, malengo yangu ni kupambana kwa ajili ya timu,” amesema Adeyum.

Nyota huyo aliyewahi kuwika na timu mbalimbali zikiwemo Yanga, Coastal Union, Stand United, Kagera Sugar na Dodoma Jiji, amesema licha ya kupata majeraha ila hayawezi kurudisha nyuma kiwango chake na ataendelea pale alipoishia.

Licha ya Adeyum kucheza beki, ameonyesha kiwango kizuri msimu huu na anashika nafasi ya pili kwa wachezaji wa Bigman waliofunga mabao mengi, akiwa na manne nyuma ya Mnigeria Collins Kelvin Nwobodo aliyefunga matano.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *