DAR ES SALAAM: MKURUGENZI wa Masoko na Mauzo Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, Seraphin Lusala, amesema jamii inapaswa kusaidiana na serikali kuhakikisha vituo vya kulelea watoto yatima vinaachana na matumizi ya kuni kwa ajili ya kupikia na kutumia nishati safi.
Amesema serikali inafanya juhudi kubwa kupunguza matumizi ya mkaa, kuni, hivyo ni wajibu wa jamii kuunga mkono.
Amesema hayo alipotembelea kituo cha kulea watoto yatima cha Maunga, kilichopo Bunju B Dar es Salaam, ikiwa ni kumbukizi ya siku ya mtoto wa Afrika, akiwa na wafanyakazi wenzake.

Lusala amesema jamii inapaswa kuendelea kujitoa kuwasaidia watoto wanaoishi vituo vya kulea watoto yatima kwamba wana mahitaji maalum na miongoni mwa mahitaji hayo ni fedha ambazo zitawawezesha kuachana na nishati chafu.
Ameeleza mkakati wa taifa ni kuhakikisha matumizi ya nishati safi katika maeneo yote na kwamba vituo vya kulelea watoto havipaswi kuachwa nyuma.
“Kila mwaka uongozi wa hoteli hiyo na wafanyakazi tulijiwekea utaratibu wa kuchangia fedha kisha kununua vifaa mbalimbali na kwenda kutembelea vituo vya watoto yatima, watu wenye uhitaji maalumu,” amesema.
Ameongeza kuwa hoteli hiyo imekuwa ikitoa msaada kwa watu wenye uhitaji maalumu kwa njia mbalimbali kutokana na uhitaji, hivyo jamii inapaswa iendelee kuwasaidia.

Kwa upande wa Katibu wa kituo cha Maunga , Alex Exaud, ameushukuru uongozi huo kutoa misaada mbalimbali ikiwa ni siku ya kumbukizi ya siku ya mtoto wa Afrika.
Katibu huyo, amesema vituo vya kulea watoto yatima, wanakuwa na mahitaji mbalimbali, hivyo wakitembelewa na wadau wanafarijika.
Ametoa wito kwa jamii kutambua na kulinda haki za watoto, kukuza upatikanaji wa elimu bora kwa watoto wote ikiwa na kauli mbiu ya mwaka huu ni Mtoto na Malezi, Msingi wa familia Bora kwa Taifa Imara.