ZURICH, USWISI. Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Kimataifa (FIFA), Gianni Infantino, amekiri kupokea simu kutoka kwa Rais wa Marekani, Donald Trump, kufuatia utata uliotokana na kadi nyekundu ya mshambuliaji, Folarin Balogun katika mechi ya Kombe la Dunia ya 2026.

Hata hivyo, Infantino amesisitiza kuwa maamuzi ya nidhamu ndani ya FIFA hayakuathiriwa na shinikizo la kisiasa, akibainisha kuwa taasisi hiyo inaendelea kufanya kazi kwa mujibu wa kanuni zake na taratibu za kisheria.

Kwa mujibu wa taarifa za ndani, Trump alimpigia simu Infantino akitaka kufanyika mapitio ya adhabu iliyotolewa kwa Balogun baada ya kadi nyekundu katika mchezo dhidi ya Bosnia na Herzegovina.

Baada ya mawasiliano hayo, Kamati ya Nidhamu ya FIFA ilipitia upya suala hilo na hatimaye kuondoa adhabu ya kufungiwa mechi moja, na badala yake kuweka adhabu ya onyo la muda (probation), hatua iliyomruhusu Balogun kucheza mchezo unaofuata dhidi ya Ubelgiji.

Akizungumzia sakata hilo, Infantino amesema, “maamuzi yote yalifanywa na vyombo huru vya nidhamu vya FIFA kwa mujibu wa kanuni zilizopo. Mawasiliano ya nje hayakuingilia mchakato wa kisheria wa shirikisho.”

Uamuzi huo umeibua mjadala barani Ulaya, ambapo Shirikisho la Mpira wa Miguu la Ubelgiji limewasilisha malalamiko rasmi, likidai kuwa uamuzi huo unahatarisha uadilifu wa mashindano.

Viongozi wa soka barani Ulaya pia wameonya kuwa kuingiliwa kwa masuala ya nidhamu na watu wa nje kunaweza kuathiri heshima ya mchezo huo duniani.

Sakata hilo sasa limeibua maswali mapya kuhusu uhuru wa FIFA katika kufanya maamuzi yake, huku mashabiki na wadau wa soka wakisubiri hatua zaidi kutoka kwa vyombo vya nidhamu vya shirikisho hilo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *