Rais wa Iran Masoud Pezeshkian amesema Marekani imegeuza Kombe la Dunia FIFA la 2026 kuwa uwanja mwingine wa uonevu na mashinikizo ya kisiasa, akisisitiza kuwa mwenendo wa Washington kama mwenyeji wa michezo hiyo unaonyesha sera zile zile inazotekeleza kote duniani.

Katika ujumbe uliochapishwa kwenye jukwaa la mitandao ya kijamii la X siku ya Jumatano, Rais Pezeshkian alisema mwenendo wa serikali ya Marekani, kama mwenyeji wa Kombe la Dunia, unaakisi sera yake ya kigeni iliyoanzishwa kwa muda mrefu.

“Mwenendo wa serikali ya Marekani kama mwenyeji wa Kombe la Dunia unafuata sera yake ya kigeni inayojulikana: kupindisha sheria, kuwadhalilisha wapinzani, kuweka vikwazo na kughushi. Huu ndio mwongozo wao wa MAGA. Iran inapinga michezo kama hiyo. Tunatetea haki zetu kwa nguvu zote,” ameandika Rais Pezeshkian.

Washington iliweka vikwazo vikubwa vya usafiri kwa timu ya taifa ya Iran, na kulazimisha kikosi hicho kubaki katika kambi yake ya mazoezi huko Tijuana nchini Mexico katika kipindi chote cha mashindano.

Timu ya soka ya Iran iliruhusiwa kuingia Marekani muda mfupi tu kabla ya mechi na ilitakiwa kuondoka ndani ya saa 24 baada ya kila mchezo, kizuizi ambacho hakuna taifa lingine shiriki lililokabiliwa nacho.

Iran iliilaani vikali Marekani na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) kuhusu hatua hizo, ikisema vikwazo hivyo vinakiuka kanuni za haki na usawa zinazotarajiwa kutoka kwa mwenyeji wa Kombe la Dunia.

Washington pia imekosolewa vikali baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kuingilia kati kwa Rais wa FIFA, Gianni Infantino kuhusu kusimamishwa mshambuliaji wa timu ya taifa ya Marekani, Folarin Balogun.

Balogun, ambaye alikuwa amesimamishwa kucheza, hatimaye aliruhusiwa kucheza dhidi ya timu ya taifa ya Ubelgiji licha ya kupewa kadi nyekundu, uamuzi uliolaaniwa na maafisa wa soka na waangalizi.

Zaidi ya wabunge 30 wa Bunge la Ulaya wametaka uchunguzi ufanyike kuhusu shinikizo la utawala wa Trump kuhusu jinsi FIFA ilivyoshughulikia kesi ya Balogun, wakisema kwamba uamuzi huo umeathiri kanuni ya kutoegemea upande wowote kisiasa kwa shirika hilo na uadilifu wa Kombe la Dunia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *