Mkurugenzi wa Huduma za Dharura katika Ukanda wa Gaza amesema kuwa takribani asilimia 80 ya uwezo wa huduma za uokoaji na misaada ya dharura umeangamizwa kutokana na mashambulizi na uharibifu unaoendelea kufanywa na utawala ghasibu wa Israel katika eneo hilo.

Fares Afana amesema uharibifu huo umeathiri kwa kiasi kikubwa uwezo wa timu za uokoaji kuwafikia waathirika, kuwatoa watu waliokwama chini ya vifusi na kutoa huduma za haraka kwa waliojeruhiwa.

Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Dharura za Tiba katika Ukanda wa Gaza amesema kuwa tangu kuanza vita vya mauaji ya kimbari katika eneo hilo, utawala wa Kizayuni umefuata sera ya kimfumo ya kulenga wafanyakazi wa huduma za dharura, magari ya uokoaji, magari ya zimamoto, hospitali na vituo vya matibabu.

Kwa mujibu wa afisa huyo, miundombinu ya huduma za dharura, magari ya uokoaji pamoja na vifaa muhimu vimeathiriwa, hali inayozidisha changamoto kwa wahudumu wa afya na uokoaji katika kuwahudumia raia.

Ameongeza kuwa hali ya kibinadamu huko Gaza inaendelea kuwa mbaya kutokana na kuendelea mashambulizi, ukosefu wa vifaa tiba na uharibifu mkubwa wa miundombinu.

Afana amesema hatua hizo ni ukiukaji wa wazi wa sheria za kimataifa na mikataba ya kibinadamu, akieleza kuwa mashambulizi dhidi ya miundombinu ya afya yameathiri pakubwa uwezo wa huduma za dharura kuwafikia majeruhi na kuokoa maisha ya wananchi.

Ameongeza kuwa kulengwa wahudumu wa afya na vifaa vya uokoaji kumesababisha kupungua kwa uwezo wa mifumo ya dharura kutoa huduma katika kipindi ambacho mahitaji ya matibabu yameongezeka kutokana na idadi kubwa ya majeruhi na uharibifu wa miundombinu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *