Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Mhandisi Zena Ahmed Said amewataka vijana nchini kujiwekea utamaduni wa kuweka akiba kupitia mifuko ya hifadhi ya jamii ili kujihakikishia usalama wa kifedha na ustawi wa maisha yao ya baadaye.
Amesema hatua hiyo itawawezesha vijana kupata huduma muhimu kama mikopo, matibabu, mafao ya uzeeni na fursa nyingine za kiuchumi zinazotolewa na mifuko hiyo.
Mhandisi Zena amebainisha hayo leo Oktoba 13, 2025 wakati akifunga Kongamano la Vijana lililofanyika kwa siku mbili jijini Mbeya.
Mhandisi Zena pia amesema vijana ndio nguvu kazi ya taifa, hivyo ni muhimu kuwekeza katika mustakabali wao kwa kupanga matumizi yao na kujiunga na mifumo rasmi ya hifadhi ya jamii.
“Kijana mwenye utamaduni wa kuweka akiba ni kijana mwenye dira ya mafanikio, anayejali kesho yake na anayechangia katika maendeleo ya taifa,” amesema.
Sambamba na hayo vijana wamehimizwa kudumisha uzalendo, kuepuka vitendo vya uvunjifu wa amani na kujiepusha na makundi yanayopandikiza chuki.
Mhariri @moseskwindi