Mwezi Agosti mwaka 2025, utabakia kuwa wa kipekee katika safari ya kisiasa ya Luhaga Joelson Mpina.

Mpina alijiunga na chama cha upinzania cha ACT Wazalendo mwanzoni mwa mwezi Agosti baada ya ‘kutoswa’ na Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika hatua za kura za maoni, akisaka jimbo la Kisesa kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Pengine wanaomfuatilia kwa makini hawakushangazwa kufuatia misimamo yake ya wazi, huku akitofautiana waziwazi na Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ndiye mwenyekiti wa CCM.

Mpina hakufurahishwa na hatua ya ‘kutelekeza’ jimbo lake kwenye masuala mbalimbali ya kimaendeleo.

Historia ya Mpina

Luhaga Joelson Mpina alizaliwa Mei 5, 1975.

Ana Shahada ya Kwanza ya Uhasibu kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe na Shahada ya Uzamili kutoka Chuo Kikuu cha Strathclyde.

Alichaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Kisesa mwaka 2005, aliendelea na nafasi hiyo kwa awamu mfululizo—2010, 2015, na 2020.

Aliteuliwa kuongoza wizara mbalimbali ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akiwa kama Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) kati ya 2015 na 2017, Waziri wa Mifugo na Uvuvi kati ya Oktoba 2017 na Juni 2020 chini ya Serikali ya Rais Magufuli.

Mwanasiasa jasiri

Mpina haraka alijizolea sifa ya kuwa mmoja wa wabunge wa CCM wenye sauti kubwa na wasio na woga, bila kukwepa kupinga maamuzi ya serikali au kudai uwazi.

Aliongoza tume mbalimbali zilizochunguza miradi na mikataba tata nchini Tanzania, ukiwemo mradi wa kuzalisha umeme wa Tegeta (IPTL), Songas, na michakato ya manunuzi.

Aliwahi kumshitaki mwanasheria mkuu wa serikali na mawaziri wa kilimo na fedha—kuhusu vibali tata vya kuagiza sukari, akiangazia matumizi mabaya ya mamlaka ya serikali.

Itakumbukwa kuwa, aliwahi kusimamishwa kuhudhuria vikao 15 vya bunge kwa kosa la kutoheshimu ofisi ya spika, wakati wa sakata la uagizaji sukari.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *