
Hii ni makala yangu ya kwanza kwa mwaka huu, 2026, hivyo naomba kuanza kwa kuwatakia heri ya mwaka mpya na kumshukuru Mungu kwa kutujalia neema kuuona mwaka.
Nauanza mwaka kwa kuidurusu sehemu ya hotuba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ya kufungia mwaka 2025 aliyoitoa siku ya mkesha wa mwaka mpya, Desemba 31, 2025, kwangu ndio mada ya kuanzia mwaka.
Kwenye hotuba hiyo, kuna vitu vingi muhimu Rais Samia amevizungumzia ila vingine muhimu zaidi, hakuvizungumzia, hivyo hii ni makala ya swali kuwa kwa mwaka 2026, kitu muhimu kuliko vyote ni kuanza kwa mchakato wa katiba mpya.
Rais Samia akilihutubia Bunge aliahidi mchakato wa katiba mpya utaanza ndani ya siku 100 za kwanza za awamu hii, lakini kwa vile mambo ni mengi zimebaki wiki chache kutimia siku 100 za kwanza, je, hili la katiba litakuwepo?
Rais Samia amezungumzia uchumi wa nchi yetu, amesema nchi yetu inaendelea kupiga hatua kubwa za kimaendeleo katika sekta mbalimbali kuboresha maisha ya watu kwa shughuli za maendeleo.
Serikali yetu imekuwa ikiendelea kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha uchumi wa Taifa, ikiwemo kudhibiti mfumuko wa bei hasa bei za bidhaa kikiwemo chakula na pato la taifa kukua kwa asilimia 6 kutoka asilimia 5.2 mwaka 2024 mpaka asilimia 5.8 mwaka 2025.
Hata hivyo, ukuaji huu wa uchumi hauakisi uchumi wa mtu mmoja mmoja, hivyo huku mtaani, hali ni ngumu.
Hali hii ya ugumu wa maisha mtaani, inatokana na ukuaji huu wa uchumi umetokana na uwekezaji wa serikali katika miradi mikubwa ya kimkakati ya miundombinu, pamoja na mchango mkubwa wa sekta za madini, ujenzi, na sekta ya fedha na huduma, ikiwemo utalii, ambako karibu kote wakandarasi ni kampuni za kigeni. Fedha zinakwenda kurejea makwao badala ya kuingia kwenye mzunguko wetu, uwekezaji wenye mrejesho mkubwa ni kwenye sekta ya kilimo ambayo ndio sekta tegemeo kwa wengi bado sio mkubwa kivile.
Kitu kizuri kuhusu mwaka huu, ni mwaka wa kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ambapo serikali itaendelea kutekeleza mkakati wa muda wa kati wa miaka mitatu (2026, 2027 na 2028), wa kuongeza mapato ya Serikali kwa kuimarisha matumizi ya mifumo ya kielektroniki katika kukusanya mapato, katika kufanya malipo na kuongeza umakini katika usimamizi wa fedha na rasilimali za umma, hili ambalo ni jambo jema.
Jambo moja kubwa linalosubiriwa kwa hamu kubwa ni kuanza kwa mchakato wa katiba mpya kama ilivyoelezwa kwenye Dira ya Taifa, na kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), ambapo Rais Samia akilihutubia Bunge, alisema mchakato huu utaanza ndani ya siku 100 za kwanza ambazo zitatimia Februari 2026, japo kwenye hotuba hii, Rais Samia hakurejelea kuanza kwa mchakato wa katiba mpya ndani ya siku 100 za kwanza, sasa kumeibuka mchakato wa kuundwa kwa tume ya maridhiano.
Hivyo, hili la mchakato wa katiba ndani ya siku 100 za kwanza sijui kama litawezekana, ila katiba mpya ndilo jambo muhimu zaidi kwa taifa letu kwa sasa kuliko jambo jingine lolote.
Si wengi wanakijua chanzo halisi cha zile vurugu za Oktoba 29, 2025 zilichangiwa na kutokufanyika kwa mabadiliko madogo ya katiba ambayo ni kitu kidogo, lakini matokeo yake ndio kile kilichotokea.
Rais Samia ametusisitiza kufanya kazi kwa bidii, mshikamano, na uzalendo, na kutimizwa kwa malengo tuliyojiwekea, kuleta uendelevu wa maendeleo yetu, hivyo serikali itachukua hatua za kimkakati kuweka mazingira rafiki ya kisera, kisheria na kiutendaji yatakayoongeza fursa za biashara, uwekezaji na fursa nyingine za kiuchumi, kijamii na kisiasa kwa Watanzania wote huku tukiendelea kuvutia wawekezaji kutoka nje ya nchi bila kusahau wajibu wetu wa kulinda rasilimali za nchi ili zitumike kwa manufaa ya Taifa.
Rais Samia amesisitiza uwepo wa utulivu wa kisiasa na hali ya amani na usalama kwa kukumbushia changamoto na mitihani iliyotugusa Oktoba 29, kwenye uchaguzi mkuu, amekiri ni tulipitia nyakati ngumu zinazohitaji subira, mshikamano na uzalendo, japo kwa maoni yangu zile vurugu zilikuwa zinaepukika kama serikali yetu ingekuwa sikivu na kusikiliza ushauri.
Rais Samia amevishukuru kwa dhati vyombo vya ulinzi na usalama na wananchi wote kwa ujumla, kwa kuendelea kudumisha amani, umoja na mshikamano wa Taifa letu. Tumeweza kuuthibitishia ulimwengu kwamba Tanzania ni Taifa imara, himilivu na lenye uwezo wa kushughulikia changamoto zake bila kuingiliwa na mataifa ya nje.
Rais Samia amesisitiza mwaka huu, Serikali imejipanga kujenga umoja wa kitaifa nchini kwa kuunda Tume ya maridhiano ambapo serikali itashirikiana na wadau wote katika kukubaliana kuhusu muundo wa Tume, aina ya wajumbe, majukumu yao na muda wa kazi wa Tume hiyo ili Watanzania turidhiane, tuwe wamoja, tusonge mbele pamoja.
Rais Samia ametoa rai kwetu sisi Watanzania, tusikubali tofauti zetu za kiitikadi, kiimani, kidini na kimitizamo zitugawe na kutupotezea malengo yetu ya maendeleo na ustawi wa Taifa letu kwa fahamu kuwa, tofauti ni sehemu ya demokrasia, lakini zisitumike kuligawa Taifa.
Rais Samia amerudia msisitizo, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi moja tu, ndani ya Jamhuri hiyo kuna uraia mmoja tu, uraia wa Tanzania na Watanzania wote ni watu wamoja ambao wamejengwa na itikadi ya kuamini kwamba amani, umoja na mshikamano hujenga uzalendo na ndio virutubisho vinavyotuletea maendeleo endelevu na ustawi wa Watanzania.
Mwaka 2026, Tanzania itaendelea kuimarisha na kudumisha ushirikiano wa kimataifa na kikanda. Vilevile, Tanzania itaendelea kutumia diplomasia ya uchumi kuvutia uwekezaji, kukuza biashara na kujenga ustawi wa watu wake, sambamba na kusimamia ulinzi wa Taifa na mchango wake katika amani na usalama barani Afrika na duniani kwa ujumla.
Moja kubwa lililonigusa ni namna Rais Samia alivyozungumzia vifo vilivyotokea mwaka 2025 kwa kusema: “Watanzania tumepoteza wapendwa wetu”.
Kauli hii ya kuwaita wote waliotangulia mbele ya haki mwaka 2025 kuwa ni wapendwa wetu ni kauli ya faraja sana, kwa Watanzania wote waliopoteza wapendwa wao, kutoka kwa Mfariji Mkuu, haijalishi hao wapendwa walikufa katika mazingira gani, binadamu wote ni sawa na ni wapendwa wetu.
Mungu Ibariki Tanzania!