Makamu wa Rais wa Iran, Mohammad Reza Aref amesema matukio ya hivi karibuni yameonyesha nguvu ya Jamhuri ya Kiislamu na kutangaza kwamba, maadui sasa wanatambua shambulio lolote dhidi ya taifa hili litawalazimu “kuomba kusitishwa kwa mapigano.”

Akizungumza katika hafla ya kuadhimisha Siku ya Posta Duniani jana Alkhamisi, Aref amesema vita vya siku 12 viliimarisha “mshikamano wa kitaifa na mtaji wa kijamii” kwa Iran.

“Sisi sio wachochezi wa vita na hatujawahi kuanzisha vita, lakini leo adui amejifunza kwamba ikiwa atatushambulia, lazima aombe makubaliano ya usitishaji vita na kutuma ujumbe,” amesema.

Aref ameongeza kuwa wakati wa mkutano na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika nchi ya kigeni, Katibu Mkuu huyo alikiri kwamba kwa vita vya siku 12, kesi ya kuanguka kwa mfumo na serikali ya Iran ilifungwa.

Makamu wa Rais wa Iran ameeleza bayana kuwa, maadui wa Iran wamekuwa wakijaribu kuiangamiza Jamhuri ya Kiislamu tangu Mapinduzi ya 1979 lakini wameshindwa, kwani kila makabiliano yameimarisha tu utulivu na umoja wa mfumo unaotawala hapa nchini.

“Hali yetu leo ​​ina nguvu zaidi na ina mshikamano zaidi kuliko miezi minne iliyopita, kabla ya vita vya kujihami vya siku 12,” Aref amesema akisisitiza kwamba, katika hali ambayo Iran haitafuti makabiliano na vita, lakini imejiandaa kikamilifu kujibu mapigo iwapo itachokozwa.

Ameongeza kuwa, uwezo wa makombora wa Iran uliomarishwa pamoja na kuwepo vikwazo dhidi ya taifa hili, ulitoa “jibu thabiti kwa utawala wa Kizayuni” wakati wa vita hivyo vya siku 12 mwezi Juni, 2025.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *