DAR ES SALAAM: Serikali ya Tanzania na Serikali ya Italia zimeanza hatua mpya ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya kilimo kwa lengo la kuongeza thamani ya mazao ya kibiashara, hususan zao la kahawa, pamoja na kuinua kipato cha wakulima nchini.

Ushirikiano huo unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa katika uzalishaji, uchakataji na upatikanaji wa masoko ya mazao ya kilimo, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa taifa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam baada ya kikao na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, amesema kuwa uwekezaji huo utajikita katika maeneo matatu muhimu ambayo ni kuimarisha usalama wa chakula, kuongeza thamani ya zao la kahawa kupitia uchakataji na matumizi ya teknolojia za kisasa, pamoja na kuimarisha upatikanaji wa mitaji kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo.

Waziri Chongolo ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kuboresha sekta ya kilimo, ambapo bajeti ya sekta hiyo imeongezwa zaidi ya mara tatu ndani ya kipindi cha miaka mitano.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *