Jeshi la Mali limesema makundi ya kigaidi yenye silaha yalishambulia ngome zake kadhaa za kijeshi katika mji mkuu Bamako mapema leo Jumamosi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Kwa mujibu wa taarifa ya jeshi, hadi tukichapisha taarifa hii, lilikuwa likiendelea kukabiliana na magaidi hao jijini Bamako na maeneo mengine.
Mwaandishi wa habari wa AP na wakazi kwa upande wao wameripoti kusikia milio ya risasi katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa nchi hiyo na katika miji kadhaa.
Kulingana na mwandishi huyo wa habari wa shirika la habari la AP jijini Bamako, milio ya silaha nzito na silaha nyengine imesikika katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Modibo Keita, karibia kilomita 15 kutoka katika Mji Mkuu Bamako. Aidha amethibitisha kuona helikopta ikipaa katika maeneo jirani.
Milio ya risasi pia imesikika katika Mji wa Kati, eneo anakotokea mkuu wa serikali ya kijeshi Assimi Goita kwa mujibu wa chanzo cha kiusalama na watu wengine walioshuhudia.
Kwenye Mji wa Gao, Mji Mkuu wa eneo la kaskazini mwa Mali, milio ya risasi pia imeripotiwa.
Mali imekuwa ikikabiliana na makundi ya kijihadi kwa zaidi ya muongo mmoja, mapinduzi ya kijeshi yakifanyika kati ya mwaka wa 2020 na 2021.
Tangu mwaka wa 2012, Mali imekabiliwa na changamoto za kiusalama kutokana na mashambulio yanayotekelezwa na makundi ya kijihadi yenye uhusiano na al- Qaeda na Islamic State pamoja na makundi mengine ya ndani yakiwemo yale yanayotaka kujitenga.
Mali sawa na jirani zake Niger na Burkina Faso ambazo pia zinaoongozwa na jeshi, imekatisha uhusiano wake na koloni yake ya zamani nchi ya Ufaransa na kuonekana kuegemea upande wa Urusi.