Kundi linalohusishwa na mtandao wa al-Qaeda na waasi wa Tuareg limedai kuhusika na mashambulizi yaliyoratibiwa kote nchini Mali siku ya Jumamosi, yanayotajwa kama mojawapo ya operesheni kali zaidi dhidi ya serikali inayoongozwa na jeshi la nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika.

Helikopta za kijeshi zilionekana zikipaa katika anga ya mji mkuu wa Mali, Bamako, na kuzunguka uwanja wa ndege wa kimataifa, huku mapigano yaliripotiwa katika kambi ya kijeshi iliyo karibu na mji huo, na kuzilazimisha balozi kadhaa za nchi za kigeni kuwashauri raia wao kubakia majumbani mwao.

Jeshi la Mali limetangaza kuwa limewaua mamia ya waasi na kuzima shambulio lililolenga maeneo mengi ndani na karibu ya mji wa Bamako, na kuongeza kuwa operesheni kubwa ya kuwasaka waasi hao inaendelea katika mji mkuu, mji jirani wa Kati ambao una kambi za kijeshi, na maeneo mengine katika nchi hiyo inayozalisha dhahabu kwa wingi.

Kundi linalojiita “Jama’at Nusrat al-Islam wal-Muslimin (JNIM)” lenye uhusiano na al-Qaeda limetoa taarifa likidai kuhusika na mashambulizi yaliyotokea katika mji wa Kati, uwanja wa ndege wa Bamako, na katika maeneo ya kaskazini, ikiwa ni pamoja na Mopti, Sévaré na Gao.

Kundi hilo pia limesema kwamba limeuteka mji wa Gao katika operesheni ya pamoja na kundi la Azawad Liberation Front, linaloongozwa na Watuareg.

Hapo awali, msemaji wa Kikosi cha Ukombozi cha Azawad, Mohamed Mouloud Ramdane, alisema kupitia mitandao ya kijamii kwamba vikosi vya kundi hilo vimechukua udhibiti wa maeneo kadhaa huko Gao, na moja ya kambi mbili huko Kidal.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *