
Mtanzania anayesoma Shahada ya Uzamivu (PhD) katika masuala ya elimu katika Chuo Kikuu cha Georgia nchini Marekani, Nichesius Godwin, amechaguliwa kuwa rais wa wanafunzi wa ngazi za uzamili na uzamivu (Masters, PhD na EdD) kupitia mtandao wa LEAP Graduate Student Network.
Uchaguzi huo unaweka historia mpya, kwani tangu kuanzishwa kwa mtandao huo miaka ya 1980, haujawahi kuwa na kiongozi mkuu kutoka bara la Afrika.
Mafanikio hayo yanaakisi juhudi, uwezo na uthubutu wa vijana wa Kitanzania katika kushiriki na kuongoza katika majukwaa ya kimataifa.
Chuo Kikuu cha Georgia kinatajwa kuwa miongoni mwa vyuo vikuu vya umma vya awali nchini Marekani, jambo linaloongeza uzito wa mafanikio hayo kwa taifa la Tanzania.
Mbali na masomo yake, Godwin pia ni Mkurugenzi wa Shirika la Domicile of Success Organization (Doso Safespace), taasisi yenye makao makuu yake jijini Mwanza, inayojihusisha na utoaji wa huduma za kielimu na kijamii kwa watoto, vijana, wanawake pamoja na watu wenye ulemavu.
Uongozi wake unatarajiwa kuimarisha uwakilishi wa wanafunzi wa kimataifa na kukuza ushirikiano wa kielimu katika mtandao huo.