Miradi yalenga kuzalisha lita bilioni 13 za maziwaMiradi yalenga kuzalisha lita bilioni 13 za maziwa

IRINGA: Katika kuadhimisha Wiki ya Unywaji Maziwa nchini inayofanyika kitaifa mkoani Iringa, Bodi ya Maziwa Tanzania imetambulisha miradi miwili mikubwa ya kimkakati inayolenga kuleta mapinduzi katika sekta ya maziwa nchini kwa kuongeza uzalishaji, kuboresha mifugo, kuimarisha usindikaji na kuongeza kipato cha wafugaji.

Miradi hiyo ni Tanzania Inclusive Processor–Producer Partnership in Dairy (TI3P) pamoja na Climate-Smart Smallholder Dairy Transformation Project (C-SDTP), ambayo kwa pamoja inalenga kuisaidia Tanzania kufikia mahitaji halisi ya maziwa ya lita bilioni 13 kwa mwaka kutoka uzalishaji wa sasa wa lita bilioni 4.2 pekee.

Hatua hiyo inaonekana kuwa mkombozi mkubwa wa sekta ya maziwa nchini, huku wataalamu wakieleza kuwa Tanzania bado ina upungufu wa zaidi ya lita bilioni tisa za maziwa kila mwaka licha ya kuwa na zaidi ya ng’ombe milioni 40.

Akizungumza wakati wa mafunzo maalumu kwa waandishi wa habari mkoani Iringa, Msajili wa Bodi ya Maziwa Tanzania, Prof George Msalya, amesema waandishi wa habari wana nafasi muhimu katika kuelimisha jamii kuhusu matumizi ya maziwa salama pamoja na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa tasnia hiyo.

Profesa Msalya amesema maziwa ni chakula muhimu na kamili kwa watu wa rika zote kutokana na kuwa na makundi yote ya virutubishi muhimu kwa mwili wa binadamu.

“Maziwa ni dhahabu nyeupe. Ni chakula cha asili na bora kwa wakati wote na kwa watu wote. Mtu anahitaji angalau glasi moja ya maziwa kwa siku na wastani wa lita 200 kwa mwaka,” amesema Profesa Msalya.

Ameonya kuwa matumizi ya maziwa yasiyokaguliwa yanaweza kusababisha madhara ya kiafya, akisisitiza umuhimu wa wananchi kutumia maziwa yaliyosindikwa na kuthibitishwa ubora wake.

Kwa mujibu wa Profesa Msalya, changamoto kubwa inayokabili sekta ya maziwa ni uzalishaji mdogo unaotokana na idadi kubwa ya ng’ombe wanaozalisha kiwango kidogo cha maziwa.

Katika kuleta mageuzi hayo, Mradi wa TI3P unaosimamiwa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa kushirikiana na Heifer International na Land O’Lakes Venture37, unalenga kuwaunganisha wafugaji na wasindikaji wa maziwa ili kuongeza tija katika uzalishaji na biashara ya maziwa.

Mwakilishi wa Benki ya Kilimo, Joseph Mabula, amesema mradi huo umewezeshwa kwa zaidi ya dola milioni 37 kwa ajili ya mikopo na uwekezaji katika sekta ya maziwa.

Amesema fedha hizo zinatumika kuwasaidia wafugaji kununua ng’ombe wa kisasa wenye tija kubwa, kujenga miundombinu ya uzalishaji pamoja na kuimarisha vituo vya ukusanyaji wa maziwa.

“Lengo letu ni kuhakikisha huduma za mikopo zinawafikia wafugaji na wasindikaji wa maziwa ili kuongeza uzalishaji na tija. Tunatekeleza mradi huu katika mikoa 15 nchini,” amesema Mabula.

Kwa upande wake, Mtaalamu wa Mnyororo wa Thamani wa Tasnia ya Maziwa, Mbehoma Peternus, amesema Mradi wa Mageuzi ya Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi (C-SDTP) ni mradi wa miaka 10 wenye thamani ya dola milioni 231 unaolenga kuboresha uzalishaji wa maziwa kwa kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira.

Amesema mradi huo utaleta ng’ombe 8,600 wenye mimba kutoka nje ya nchi ambapo 600 watapelekwa Zanzibar huku wengine wakisambazwa katika maeneo mbalimbali nchini ili kuanzisha kizazi kipya cha wafugaji wenye tija.

“Mwisho wa mradi tunatarajia kuwa na zaidi ya ng’ombe 24,500 wa kisasa watakaozalishwa hapa nchini na kuongeza kwa kiwango kikubwa uzalishaji wa maziwa,” amesema Peternus.

Ameongeza kuwa mradi huo pia utajenga vituo vingi vya kisasa vya kukusanyia maziwa, ambapo asilimia 50 vitajengwa katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Kwa mujibu wa Peternus, mradi huo unatarajiwa kunufaisha kaya zaidi ya 140,000 sawa na wananchi takribani 700,000, huku wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalumu wakipewa kipaumbele maalumu.

Mbali na miradi hiyo miwili mikubwa, Bodi ya Maziwa Tanzania imeeleza kuwa kuna miradi mingine inayoendelea nchini ikiwemo mradi wa kuimarisha mfumo wa ukusanyaji maziwa wenye thamani ya zaidi ya Sh Bilioni 452, pamoja na miradi inayolenga kuongeza thamani ya bidhaa za maziwa, matumizi ya nishati jadidifu na uwekezaji katika usindikaji wa mtindi na bidhaa nyingine za maziwa.

Wanahabari walioshiriki mafunzo hayo wameeleza kuwa elimu waliyoipata itawasaidia kuhamasisha jamii kutumia maziwa salama na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa sekta ya maziwa katika kukuza uchumi wa taifa na kuboresha afya za wananchi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *