
Dar es Salaam. Wakazi wawili wa Mburahati kwa Jongo, Abubakar Naseeb (41) na Stara Kombo (35) wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kujibu shtaka moja la kusafirisha gramu 640 za dawa za kulevya aina ya bangi.
Washtakiwa hao wamefikishwa Mahakama hapo leo Ijumaa Mei 29, 2026 na kusomewa kesi ya jinai namba 11851/2026 na wakili wa Serikali Mwandamizi, Theresia Mtao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Dk Salome Mshasha.
Wakili Mtao amedai washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa Septemba 12, 2025 eneo la Mburahati kwa Jongo, lililopo Wilaya ya Kinondoni, walikutwa wakisafirisha dawa za kulevya aina ya bangi zenye uzito wa gramu 640, kinyume cha sheria.
Washtakiwa baada ya kusomewa shtaka lao, walikana kutenda kosa hilo.
Upande wa Jamhuri ulidai upelelezi umekamilika hivyo, wanaomba tarehe kwa ajili kuwasomea hoja za awali.
“Mheshimiwa hakimu, upelelezi umekamilika hivyo tunaomba tupangiwe tarehe nyingine kwa ajili ya kuwasomea hoja za awali washtakiwa hapa. Pia, kiasi cha dawa wanachodaiwa kusafirisha kina dhamana kama watatimiza masharti ya dhamana” amedai Mtao.
Hakimu Mshasha baada ya kusikiliza hoja hizo alitoa masharti matatu ya dhamana dhidi ya washtakiwa hao.
Kwanza, alitaka kila mshtakiwa awe na wadhamini wawili ambao ni wakazi wa mkoa wa Dar es Salaam.
Pili, wadhamini hao wanatakiwa kusaini fungu la dhamana lenye thamani ya Sh10 milioni.
Vilevile, wadhamini hao wanatakiwa wawe na barua za utambulisho kutoka serikali za mitaa au barua za ajira kama ni watumishi.
Washtakiwa wamefanikiwa kupata dhamana na kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 12, 2026
