LIGI Kuu ya Wanawake Tanzania Bara imesogezwa mbele ili kupisha kalenda ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) kwenye michuano ya kimataifa ya Three Nations Tournament itakayofanyika kuanzia Juni 1 hadi 9 mwaka huu, jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa, ligi hiyo itasimama kwa siku 11 mara baada ya kukamilika kwa mechi za raundi ya 20 na  jumla ya mechi sita zimechezwa jana.

Hatua hiyo inalenga kutoa nafasi kwa Timu ya Taifa ya Wanawake Tanzania, Twiga Stars kufanya maandalizi na kushiriki mashindano hayo ya Three Nations Tournament.

Mashindano hayo yatazikutanisha timu tatu za taifa ambazo ni Tanzania, Ghana na Malawi, yakitarajiwa kutumika kama sehemu ya maandalizi ya mechi na mashindano yajayo.

Baada ya kumalizika kwa michuano hiyo, Ligi Kuu ya Wanawake itarejea Juni 12 kwa mechi za raundi ya 21 na 22 ambayo ndiyo itahitimisha rasmi msimu wa 2025/26.

Kusimamishwa kwa ligi hiyo kunakuja wakati ushindani ukiwa mkubwa katika mbio za ubingwa pamoja na vita ya kujiokoa na kushuka daraja, hali inayofanya kila mechi zilizosalia kuwa na umuhimu mkubwa kwa timu zinazowania malengo tofauti.

Hadi sasa Simba Queens inaongoza ligi ikiwa na pointi 53 tofauti ya pointi 10 na Yanga Princess iliyopo nafasi ya pili na pointi 43 huku JKT Queens ikiwa nafasi ya tatu na pointi 42.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *