
Baada ya siku nzima ya ushindani mkali, Tamasha la Touch Rugby Tournament limefikia tamati kwa kushuhudia mechi za fainali za mchezo wa raga, zilizovutia mashabiki wengi waliojitokeza kwenye Uwanja wa Ufundi, Mikocheni, jijini Dar es Salaam.
Katika fainali ya kundi la watoto, timu ya Iringa ilionyesha ubora mkubwa na kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Tanga, matokeo yaliyoiwezesha kutwaa ubingwa wa kundi hilo na kuondoka na kombe.
Kwa upande wa wakubwa, fainali ilikuwa na ushindani mkubwa huku Iringa ikikabiliana na Kenya katika mechi iliyokuwa na kasi na mvuto mkubwa. Iringa iliibuka na ushindi wa mabao 3-2 baada ya pambano kali lililowafanya mashabiki kubaki kwenye viti vyao hadi dakika za mwisho.
Kutokana na ushindi huo, Iringa ilikabidhiwa kombe la ubingwa huku wachezaji na benchi la ufundi wakishangilia mafanikio hayo mbele ya mamia ya watazamaji waliohudhuria tamasha hilo.
Mbali na mechi za fainali, mashindano hayo yalileta pamoja timu kutoka maeneo mbalimbali ya Afrika Mashariki, jambo lililoonyesha ukuaji wa mchezo huo na kuongeza ushirikiano wa kimichezo katika ukanda huo.
Waandaaji wa mashindano hayo, Dar Leopards RFC, walieleza kuridhishwa na mafanikio ya tamasha hilo na ushiriki mkubwa wa timu, mashabiki na wadhamini umeifanya toleo la mwaka huu kuwa miongoni mwa yaliyoacha alama kubwa tangu kuanzishwa kwake.
Tamasha hilo lilihitimishwa kwa utoaji wa makombe, medali na tuzo mbalimbali kwa washindi pamoja na washiriki walioonyesha kiwango bora, huku waandaaji wakiahidi kurejea tena mwakani kwa tamasha kubwa zaidi.