- Seneta Edwin Sifuna anapanga kupinga mahakamani uondolewaji wake katika nafasi ya Katibu Mkuu wa ODM
- Kundi la Sifuna linadai uamuzi wa ODM unakiuka haki za kikatiba na una dosari kisheria
- Mzozo huo wa kisheria unazidisha mpasuko ndani ya chama cha ODM, huku Sifuna akipambana kuilinda nafasi yake
Seneta Edwin Sifuna ametangaza kuwa atapinga mahakamani uamuzi wa Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) wa kumwondoa katika wadhifa wa Katibu Mkuu wa chama hicho.
Akizungumza wakati wa mkutano na wanahabari ulioitishwa Jumanne asubuhi na mrengo wa “Linda Mwananchi” jijini Nairobi, Sifuna na washirika wake walitaja hatua ya hivi karibuni ya Kamati Kuu ya Kitaifa ya Utendaji ya ODM (NEC) kuwa ni kinyume cha Katiba, wakiahidi kuipinga kupitia njia za kisheria.
Katika taarifa iliyosomwa na Mbunge wa Suba Kusini, Caroli Omondi, mrengo huo uliushutumu uongozi wa chama kwa kurudia makosa yale yale ambayo hapo awali yaliifanya Mahakama ya Migogoro ya Vyama vya Kisiasa kubatilisha jaribio la awali la kumwondoa Sifuna.
“Jana usiku tulifahamishwa kuhusu uamuzi wa NEC ya ODM unaodai kwa mara ya pili kumwondoa Katibu Mkuu Edwin Sifuna kutoka ofisini. Kwa mtazamo wa kwanza, uamuzi huo unafanana na ule uliofanywa mwezi Februari ambao haukuwa wa haki na ulikuwa kinyume cha Katiba,” alisema Omondi.
Mrengo huo ulisisitiza kuwa uamuzi huo mpya una mapungufu ya kisheria.
Walieleza kuwa wana imani kamili kwamba mahakama itatoa tena uamuzi unaomuunga mkono Sifuna na kubatilisha agizo hilo la chama.
“Tumedhamiria kupima uhalali wa kuondolewa huko kunakodaiwa mahakamani kwa sababu tunaamini kutakumbwa na hatima ile ile iliyolikumba jaribio la mwezi Februari,” aliongeza Omondi.
Kadiri vita hivi vya kisheria vinavyozidi kupamba moto, mgawanyiko ndani ya chama hicho cha upinzani unaendelea kuongezeka huku Sifuna akitafuta rasmi kuzuia nafasi yake kuchukuliwa na kuhakikisha anasalia katika wadhifa huo.
Read ENGLISH VERSION
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.
Chanzo: TUKO.co.ke
