
Mkuu wa shirika lisilo la kiserikali la Palestina huko Gaza ameripoti kuongezeka kwa mgogoro wa kibinadamu katika Ukanda wa Gaza.
Amjad Al-Shawa, mkuu wa Mtandao wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya Palestina katika Ukanda wa Gaza, ameiambia Kanali ya Televisheni ya Al Jazeera kwamba hali ya kibinadamu kwa wakazi wa eneo hilo imekuwa ngumu na ngumu zaidi.
Mkuu wa Mtandao wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya Palestina aliongeza kuwa angalau watu 18,500 wanahitaji matibabu ya haraka nje ya Gaza.
Amjad Al-Shawa aliendelea kusema kwamba asilimia 90 ya wakazi wa Ukanda wa Gaza wanategemea moja kwa moja misaada ya kibinadamu, na vikwazo vinavyoendelea vimeyafanya maisha ya kila siku ya watu kukabiliwa na mgogoro mkubwa.
Alisema kwamba idadi kubwa ya watoto wa Kipalestina wameambukizwa magonjwa yanayohusiana na mafua, na baadhi wamepoteza maisha kutokana na mafua hayo.
Mkuu wa Mtandao wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya Palestina ametoa wito wa shinikizo kwa wavamizi kufungua vivuko na kuruhusu misaada ya kibinadamu ya haraka kuingia Ukanda wa Gaza. Aliwataka, wajumbe maalum wa Trump, kuchukua hatua za vitendo na za haraka ili kurahisisha utoaji wa misaada na kupunguza mateso ya watu wa Gaza.
Hayo yanajiri katika hali ambayo, Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema zaidi ya Wapalestina 1,000 wamepoteza maisha katika Ukanda wa Gaza kati ya Julai 2024 na Novemba 2025, wakisubiri ruhusa ya utawala wa Israel kuhamishwa kwa ajili ya matibabu kutoka kwa mamlaka za Kizayuni.