Rais wa Jamhuri ya Kongo, Denis Sassou-Nguesso, na wasaidizi wake wanadaiwa kuhusishwa na rushwa ya kiasi “cha juu zaidi” kuhusiana na utoaji wa vibali vya mafuta, kulingana na taarifa iliyotolewa siku ya Jumatatu, Januari 26, huko Oslo, na Mamlaka ya Uhalifu wa Kiuchumi ya Norway. Mwendesha mashtaka anayesimamia kesi hiyo alitangaza mashtaka ya “ufisadi uliokithiri” dhidi ya raia wawili wa Norway na kampuni tanzu ya kampuni ya mafuta ya Norway Petronor.

Imechapishwa: Imehaririwa:

Dakika 2 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Yote yalianza na muamala ulioonekana kuwa “wa kutiliwa shaka” unaohusisha benki ya Monegasque. Kitengo cha Ujasusi wa Fedha cha Monaco kisha kikafungua uchunguzi na kuomba msaada kutoka Norway.

Ofisi ya Upelelezi wa Jinai ya Norway (Okokrim), mamlaka ya Norway inayohusika na mashtaka ya uhalifu wa kiuchumi, imechukua kesi hiyo na kusema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kwamba imepokea usaidizi “mkubwa” kutoka nchi kadhaa katika uchunguzi wake, ikiwa ni pamoja na Marekani na Ufaransa. Imefichua kesi ya “ufisadi mkubwa.”

Kwa hivyo, ofisi ya mwendesha mashtaka wa umma ya Norway imetoa mashtaka dhidi ya raia wawili wa Norway na kampuni waliyoifanyia kazi, Hemla Africa Holding, kampuni tanzu inayomilikiwa kikamilifu na kapmuni ya Norway ya Petronor E&P, iliyoorodheshwa kwenye Soko la Hisa la Oslo.

Mashtaka hayo yanahusiana na malipo ya rushwa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita nchini Jamhuri ya Kongo, kuhusiana na maombi na utoaji wa vibali vya mafuta katika nchi hii ya Afrika ya Kati.

Kampuni ya Kongo ya MGI International, inayodhibitiwa na watu wa karibu wa familia ya rais, ilikuwa na hisa ya 25% katika kampuni yenye leseni ya ndani, Hemla E&P Congo (HEPCO), huku Hemla Africa Holding ikishikilia asilimia 75 iliyobaki.

Raia hao wawili kutoka Norway “walihakikisha kwamba […] gawio lililipwa mara kwa mara na HEPCO kwa MGI. Hadi mwaka 2024 ukijumuishwa, hii ilimpa rais faida ya angalau dola milioni 24.68 kupitia wanafamilia wake wa karibu,” mashtaka hayo yanasema.

Petronor “inapinga mashtaka dhidi ya Hemla na inakaribisha fursa ya kesi hiyo kuchunguzwa kwa kina mahakamani,” kampuni hiyo imesema katika taarifa.

Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai ya Norway (Okokrim) inabainisha kuwa malipo haya yanahusiana na Rais wa Kongo na wanafamilia wake wa karibu. Hata hivyo, mamlaka ya Norway haina mamlaka zaidi ya mipaka yake na kwa hivyo haiwezi kupanua uchunguzi wake kwa wale wanlioweza kunufaika na rushwa hizi.

Mamlaka ya Kongo bado haijajieleza kuhusiana na tuhuma hizi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *