
Unguja. Wanafunzi wawili wa mwaka wa kwanza wa shahada ya awali ya Mawasiliano ya Umma katika Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (Suza) wamefariki dunia wakati wakiogelea baharini.
Wanafunzi hao, Thobias Chikakalanga, mkazi wa Dar es Salaam na Hamza Fakih kutoka Mtwara waliokuwa wakisoma kampasi ya Habari Kilimani, walifariki jana Mei 16, 2026 jioni katika pwani ya Kizigo walikokwenda kuogelea.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Richard Mchomvu amethibitisha vifo hivyo, akisema atatoa taarifa yake baadaye.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Mei 17, 2026 na Serikali ya Wanafunzi ya Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (Suzaso) kupitia Katibu Mkuu wake, Mulhat Muhsin Swaleh, wanatoa pole kwa familia za marehemu, uongozi wa Suza, walimu na wanafunzi wote.
“Serikali ya wanafunzi inaungana na jamii ya Suza katika maombolezo kuwaombea marehemu wapumzike kwa amani,” amesema.
Kwa mujibu wa shuhuda wa tukio hilo, (ambaye hakutaka jina lake kutumika) ameeleza kuwa wanafunzi hao walipomaliza kufanya kipindi jana jioni katika redio ya Habari Fm, walikwenda Pwani Kizigo kuogelea. Wakiwa wanne, mwenzao mmoja akasema hajui kuogelea, akawashikia nguo zao.
Watatu wakaingia kwenye maji, mmoja akarudi akipiga kelele akisema hawaoni Thobias na Hamza, wamezama majini.
“Baadaye, Thobias akapatikana akiwa ameshafariki na Hamza naye akapatikana akiwa mzima mwenye hali mbaya, akapelekwa hospitali lakini baadaye naye alifariki.”
