Rais wa Ecuador Daniel Noboa amenusurika kifo baada ya gari lake kushambuliwa alilokuwa akisafiria kusini mwa nchi hiyo. Shambulio hilo limekuja huku kukiwa na maandamano makali ya watu wa asili, serikali yake imetangaza tarehe 7 Oktoba.

Imechapishwa:

Dakika 1 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Huko Cañar, kusini mwa Ecuador, “watu 500 walitokea na kuanza kurusha mawe kwenye msafara wa rais, na ni wazi, pia kuna matundu ya risasi kwenye gari la rais,” Waziri wa Mazingira na Nishati wa Ecuador Inés Manzano amewaambia waandishi wa habari, na kuwahakikishia rais hakujeruhiwa.

Kwenye mtandao wa kijamii wa X, ofisi ya rais imeeleza kuwa ni “shambulio” na ikatoa video zinazoonyesha tukio hilo kutoka ndani ya gari moja kwenye msafara wa rais, huku mabomu kadhaa yaliyotengenezwa kienyeji yakigonga madirisha na mtu aliyekuwa ndani akipiga kelele “inamisheni vichwa vyenu.” Picha nyingine zilizochukuliwa nje zilionyesha kundi la waandamanaji, wengine wakiwa wamevalia mavazi ya kitamaduni, wakirusha mawe na fimbo kwenye msafara huo.

Mamlaka inachunguza iwapo athari zinazoonekana kwenye gari aina ya SUV lisiloingiza risasi lililokuwa limembeba kiongozi huyo zilisababishwa na urushaji risasi. Msafara wa magari ulilengwa ulipokuwa ukielekea katika mji wa Andean wa Cañar (kusini mwa Ecuador). Rais wa kihafidhina kisha ameshiriki katika hafla ya umma katika jiji la Cuenca, ambapo amefutlia mbali “mashambulizi haya, ambayo hayakubaliki katika Ecuador mpya.” “Sheria inatumika kwa kila mtu. Hatutaruhusu waharibifu wachache kutuzuia kufanya kazi kwa ajili yenu,” ameambia hadhira.

Inés Manzano ameripoti kwamba serikali iliwasilisha malalamiko kwa “jaribio la mauaji” na kwamba watu watano wamekamatwa. Watachunguzwa kwa kosa la ugaidi, adhabu yake ni kifungo cha hadi miaka 30 jela.

Maandamano ya watu wa asili

Tangu Septemba 22, serikali ya Noboa imekuwa ikikabiliwa na maandamano yaliyoambatana na vizuizi vya barabarani katika majimbo kadhaa, yaliyoitishwa na shirika kubwa la watu wa asili nchini humo (Conaie), ili kukabiliana na kuondolewa kwa ruzuku ya dizeli, ambayo iliongeza bei kutoka dola 1.80 hadi dola 2.80 kwa dumu (lita 3.8).

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *