Vijana waandamanaji nchini Madagascar siku ya Jumatano walikataa ombi la kujiunga na “mazungumzo ya kitaifa” ya Rais Andry Rajoelina na makundi mbalimbali, wakiishutumu serikali yake kwa ukandamizaji baada ya wiki kadhaa za maandamano katika taifa hilo la visiwa vya Afrika.
Kwa kuchochewa na vuguvugu kama hilo la “Gen Z” nchini Kenya na Nepal, maandamano yaliyoanza Septemba 25 yanaleta changamoto kubwa kwa serikali ya Rajoelina tangu kuchaguliwa tena mwaka 2023, na kutoa sauti ya kutoridhika kwa watu wengi kutokana na kukithiri kwa umaskini na ufisadi wa hali ya juu.
Rais Rajoelina alilifuta baraza lake la mawaziri wiki iliyopita kwa nia ya kuzima machafuko hayo, akimteua waziri mkuu mpya na kutangaza mipango ya mazungumzo ya kitaifa yanayotarajiwa kuanza Jumatano alasiri.
Alisema mazungumzo hayo yatahudhuriwa na viongozi wa kiroho, wanafunzi, wawakilishi wa vijana na wengine.
Lakini hatua hizo zimeshindwa kupunguza hasira ya umma, na wale wanaojiita vuguvugu la Gen Z walisema hawatafanya mazungumzo na serikali mradi tu mamlaka itajibu maandamano yao kwa nguvu.
“Tunakataa dhihaka hii ya mazungumzo,” waandamanaji walisema kwenye taarifa iliyochapishwa kwenye ukurasa wao wa Facebook ulioidhinishwa.
“Tunakataa mualiko wa rais kwenye mazungumzo. Hatutashiriki katika mazungumzo na utawala unaokandamiza, kuwashambulia na kuwadhalilisha vijana wake mitaani.”
Wanafunzi wa chuo kikuu walitarajiwa kuingia mitaani tena Jumatano kufuatia makataa ya saa 48 yaliyotolewa na waandamanaji Jumatatu usiku kwa Rajoelina kukubaliana na matakwa yao la sivyo akabiliane na mgomo wa kitaifa.