Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres katika ujumbe wake wa siku hii ameonya kwamba migogoro huwaathiri zaidi wasichana, wanaokabiliana na hatari kubwa za ukatili wa kijinsia, vifo vya uzazi, na ndoa za utotoni.

Amesema “Dunia yetu imezungukwa na migogoro. Wakati migogoro inapoibuka, wasichana mara nyingi wanalipwa gharama kubwa zaidi,” Guterres

Ameongeza kuwa “Lakini wasichana pia wanaongoza kwenye suluhu. Hali ya sasa inaonesha kwamba wanachukua hatua katika masuala ya haki za kijinsia, elimu, hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, na mengi zaidi. Lazima tuwaunge mkono, tuweke kipaumbele kwa haki zao, na tuwekeze katika fursa zao.”

Maendeleo na changamoto zilizopo

Sherehe hizi zinatokea miaka 30 baada ya kupitishwa kwa Tamko la Beijing, kielelezo cha kihistoria cha usawa wa kijinsia. Ingawa maendeleo yapo, ukosefu wa usawa bado upo.

Ripoti ya pamoja ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, Shirika la Umoja wa mataiifa la Masuala ya Wanawake UN Women, na Plan International, iliyopewa jina “Malengo ya Wasichana: Nini Kinabadilika kwa Wasichana?”, inaonesha kwamba wasichana walioko kwenye mazingira hatarishi bado wanakabiliana na vikwazo katika elimu, afya, na uwezeshaji.

“Watoto wa kike wa miaka ya ujana wana uwezo wa kubadilisha dunia, lakini tuwaunge mkono kwa elimu, fursa salama, na fursa za kuongoza,” Guterres ameongeza katika ujumbe wake. “Kila mtoto wa kike, kila mahali, anastahili usawa, fursa, na heshima.”

Wasichana wanaongoza hatua za tabianchi na jamii

Duniani kote, wasichana wanaonekana zaidi kama viongozi wa mabadiliko. Mwanaharakati wa tabianchi kutoka Uganda, Vanessa Nakate, mwanzilishi wa Rise Up Movement, alisisitiza jinsi majanga ya mazingira yanavyohusiana na jinsia.

“Wasichana na wanawake barani Afrika wanabeba mzigo mkubwa wa majanga ya tabianchi, lakini pia wanaongoza suluhu katika jamii zao,” Nakate alisema. “Tunahitaji sera na ufadhili unaothamini michango yao na kushughulikia changamoto wanazokabiliana nazo.”

Wito wa kuchukua hatua

Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanaomba serikali, jamii, na watu binafsi kuwaunga mkono watoto wa kike kwa kusambaza hadithi zao, kupigania haki zao, na kuunda nafasi salama zinazotegemea usichana.

Uwekezaji katika elimu, afya, na ustawi wa kisaikolojia wa wasichana unachukuliwa si tu kama jukumu la kimaadili bali pia ni muhimu kwa kujenga jamii zenye amani na maendeleo.

“Kwa miaka mitano tu iliyobaki kufanikisha Malengo ya Maendeleo Endelevu  SDGs ya 2030, kuunga mkono watoto wa kike ni muhimu,” amesema Guterres. Amehitimisha kwa kusema kuwa “Wasichana hawasubiri dunia bora wanaiunda. Ni jukumu letu kusikiza sauti zao, kulinda haki zao, na kufungua uwezo wao kamili.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *