DAR ES SALAAM: Mwanamitindo wa kimataifa, Flaviana Matata, amewataka Watanzania kujivunia na kupenda bidhaa za ndani ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi.
Akizungumza na waandishi wa habari, Flaviana amesema kuwa kama balozi wa chapa, anaamini katika ubora na hawezi kuhusisha jina au sura yake na bidhaa zisizofikia viwango vya kimataifa.
Katika kuimarisha chapa yake, kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL) imemtangaza rasmi Flaviana kuwa balozi wake wa kimataifa. Uteuzi huo unalenga kuunganisha biashara na taswira ya Tanzania ya kisasa, inayojitegemea na yenye kujiamini.
Flaviana amesisitiza kuwa umefika wakati kwa Tanzania kutambulika kama nchi inayozalisha bidhaa zenye ubora wa kimataifa.
Amebainisha kuwa mafanikio hayo yanawezekana ikiwa Watanzania wataendelea kupenda na kuunga mkono bidhaa za nyumbani zenye ubora wa juu.

Aidha, ameeleza kuwa kuunga mkono bidhaa za ndani kunasaidia kukuza ajira kwa wazalishaji, wabunifu na wauzaji, huku pia kukichochea ubunifu katika sekta mbalimbali.
Akizungumzia uzinduzi wa bidhaa mpya, Flaviana amesema safari ya kuelekea Serengeti National Park ni sehemu ya mkakati wa kukuza utalii na kuonesha fahari ya Tanzania kimataifa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Obinna Anyalebechi, amesema uzalishaji wa bidhaa za ndani una mchango mkubwa kiuchumi, ikiwemo kuongeza ajira, kuimarisha mnyororo wa thamani na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje.
Ameongeza kuwa hatua hiyo pia inaongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.
SBL imezindua kinywaji kipya cha Serengeti Premium Apple, bidhaa ya kwanza ya aina ya Ready-to-Drink (RTD) kutengenezwa nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza viwanda vya ndani na kuongeza thamani ya bidhaa za Kitanzania.
Uzinduzi rasmi wa bidhaa hiyo unatarajiwa kufanyika katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, tukio linalotarajiwa kuvutia wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.