JKCI kuanza kupandikiza moyoJKCI kuanza kupandikiza moyo

TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imeanza mchakato wa kuanzisha huduma za upandikizaji wa moyo nchini, hatua inayolenga kuboresha huduma za matibabu ya magonjwa ya moyo na kuiweka Tanzania katika ramani ya huduma za kibingwa duniani.

Akizungumza leo Aprili 9, 2026 jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Peter Kisenge, amesema taasisi hiyo ilifanya upembuzi yakinifu mwaka 2025 na kuunda kamati maalumu iliyoweka dira ya utekelezaji wa huduma hiyo.

Amesema kamati hiyo imekamilisha kazi yake na kukabidhi rasimu ya muongozo wa uanzishwaji wa huduma za upandikizaji wa moyo mwezi Januari mwaka huu, huku hatua inayofuata ikiwa ni kuwapeleka wataalamu wa JKCI katika hospitali kubwa duniani kwa ajili ya mafunzo na kujifunza uzoefu wa huduma hizo. SOMA: JKCI yazindua kampeni magonjwa yasiyoambukiza

Ameeleza kuwa lengo la JKCI ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 taasisi hiyo inakuwa miongoni mwa hospitali zinazotoa huduma ya upandikizaji wa moyo duniani. Katika hatua nyingine, Dk. Kisenge amesema Serikali ya Awamu ya Sita imewekeza katika ujenzi wa maabara ya kisasa na kubwa zaidi Afrika Mashariki na Kati, inayotumia teknolojia ya akili mnemba (AI) na mfumo wa kiroboti katika uchakataji wa sampuli za vipimo.

Ameongeza kuwa uwekezaji huo umeongeza ufanisi kwa kupunguza makosa ya kibinadamu na kupunguza muda wa kupata majibu ya vipimo kutoka saa tatu hadi saa moja. Aidha, amesema maabara hiyo ina uwezo wa kutambua magonjwa katika hatua za awali na kuchakata idadi kubwa ya sampuli kwa muda mfupi, hatua inayochangia kuboresha huduma kwa wagonjwa na kupunguza muda wa kusubiri hospitalini.

Dk. Kisenge ameongeza kuwa maabara hiyo imeifanya JKCI kuwa kitovu cha ubora wa huduma za uchunguzi katika ukanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Afrika Mashariki, huku pia ikitumika kama kituo cha mafunzo kwa wataalamu wa afya na utafiti wa kitabibu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *