Kwa zaidi ya mwongo mmoja, mijadala katika Mkutano wa Afya Tanzania (Tanzania Health Summit – THS) imekuwa ikirudia swali moja la msingi: Tanzania itawezaje kufungua fursa za uwekezaji wa sekta binafsi ili kujenga mfumo wa afya imara, unaojitegemea?

Leo, mijadala hiyo haibaki tena ndani ya kumbi za mikutano pekee. Inaonekana wazi katika sera za kitaifa na mwelekeo wa kisiasa wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2014, Mkutano wa Afya Tanzania umekuwa jukwaa linalowakutanisha watunga sera, wawekezaji, wataalamu wa afya na wadau wa maendeleo kujadili mustakabali wa ufadhili wa sekta ya afya, ubunifu na ukuaji wa viwanda vya afya.

Mikutano ya awali ilisisitiza ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi kama chachu ya mageuzi ya mfumo wa afya.

Kufikia katikati ya miaka ya 2010, mijadala ilikomaa na kuelekeza nguvu zaidi kwenye utekelezaji wa bima ya afya kwa wote kupitia juhudi za pamoja za sekta ya umma na binafsi, pamoja na umuhimu wa kimkakati wa uzalishaji wa ndani wa dawa na vifaa tiba.

Mwaka 2017 na 2018, majadiliano ya THS yalizidi kuimarika kuhusu uviwandishaji wa sekta ya afya, yakichambua kwa kina namna uzalishaji wa ndani wa dawa ungepunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje, kuboresha uhakika wa upatikanaji wa bidhaa za afya na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Hoja hizi ziliendelezwa katika miaka iliyofuata, huku mada za mkutano zikisisitiza ufanisi, uendelevu, ubunifu na mchango wa mitaji binafsi katika kuimarisha mifumo ya afya.

Katika matoleo ya hivi karibuni, ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi haujaonekana tena kama nyongeza ya hiari, bali kama nguzo muhimu ya utoaji wa huduma bora na zenye usawa.

Majadiliano haya ya muda mrefu sasa yanaakisiwa wazi katika kauli za hivi karibuni za Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa.

Katika hotuba na matamko mbalimbali yaliyotolewa kupitia majukwaa rasmi ya serikali na mitandao ya kijamii, Waziri amesisitiza kuwa uzalishaji wa ndani wa dawa, vifaa tiba na teknolojia za afya si ndoto ya baadaye tena, bali ni kipaumbele cha sasa cha kitaifa.

Amebainisha kuwa Tanzania inachukua hatua za makusudi kupunguza utegemezi mkubwa wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, na badala yake kujenga uwezo wa uzalishaji wa ndani unaokidhi viwango vya kimataifa vya ubora.

Kwa mujibu wa waziri, Serikali imevuka hatua ya majadiliano na kuingia kwenye utekelezaji.

Hatua zilizotangazwa ni pamoja na kuharakisha taratibu za idhini za udhibiti kwa wazalishaji wa bidhaa za afya, kuratibu msaada wa uwekezaji kati ya taasisi mbalimbali za Serikali, na kutoa mwaliko wa wazi kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kuanzisha viwanda vya uzalishaji wa dawa na vifaa tiba nchini Tanzania.

Msingi wa mkakati huu ni msisitizo kwamba uzalishaji wa ndani lazima ushindane kwa ubora, usalama na ufanisi, kwa kuzingatia viwango vya kimataifa huku ukihudumia mahitaji ya Taifa.

Wachambuzi wa sekta ya afya wanaeleza kuwa mwelekeo huu wa sera unaendana kwa karibu na hoja ambazo zimekuwa zikisisitizwa mara kwa mara katika Mkutano wa Afya Tanzania.

Kuanzia wito wa kuendeleza viwanda vya dawa kama sehemu ya utekelezaji wa bima ya afya kwa wote, hadi mijadala kuhusu ufanisi wa mifumo ya afya na ufadhili endelevu, THS imekuwa ikisisitiza kuwa uviwandishaji hauwezi kutenganishwa na usalama wa afya.

Mkutano huu kwa muda mrefu umeona uzalishaji wa ndani si tu kama fursa ya kiuchumi, bali kama hitaji la kimkakati kwa ajili ya ustahimilivu wakati wa misukosuko ya ugavi, majanga ya kiafya na mishtuko ya masoko ya kimataifa.

Kadri nchi inavyojiandaa kwa mkutano ujao wa Pharmaceutical Production and Investment Forum unaotarajiwa kufanyika Januari 19, 2026, wadau ndani ya jumuiya ya THS wanasema wakati huu unaashiria muunganiko wa maono na utekelezaji.

“Tunachokiona sasa ni tafsiri ya miaka mingi ya majadiliano kuwa dhamira thabiti ya serikali,” alisema mchambuzi mmoja wa sekta ya afya. “Msisitizo wa uviwandishaji si jambo jipya, lakini nguvu na uwazi wa uungwaji mkono wa kisiasa ni wa kipekee.”

Bodi na Menejimenti ya Mkutano wa Afya Tanzania wamepokea kwa furaha mwelekeo huu chanya, wakieleza kuunga mkono kikamilifu msukumo mpya wa serikali kuelekea uviwandishaji wa sekta ya afya.

Wameeleza kuwa jukumu la Mkutano daima limekuwa ni kutoa majadiliano yanayotegemea ushahidi, kuwakutanisha wadau mbalimbali, na kusaidia kulinganisha vipaumbele vya kitaifa na uwezo wa sekta binafsi. Msimamo wa sasa wa sera, wanasema, unaonesha thamani ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya serikali, sekta binafsi na wataalamu wa afya.

Kadri Tanzania inavyosonga mbele kuelekea kujitegemea zaidi katika uzalishaji wa bidhaa za afya, ulinganifu kati ya uongozi wa kitaifa na majukwaa kama Mkutano wa Afya Tanzania unaashiria mabadiliko makubwa: Kutoka mjadala wa sera kwenda kwenye hatua za pamoja za utekelezaji.

Endapo mwelekeo huu utaendelea, unaweza kuwa hatua muhimu ya mabadiliko katika namna nchi inavyofadhili, kuzalisha na kutoa huduma za afya, na kuufanya uviwandishaji kuwa nguzo kuu ya mustakabali wa sekta ya afya.

Dk Omary Chillo ni Rais wa Mkutano wa Afya Tanzania (Tanzania Health Summit)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *