WAANDISHI bunifu kutoka ndani na nje ya Tanzania wanatarajiwa kuchuana kuwania Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu 2026, huku mshindi akitarajiwa kujinyakulia hadi Sh milioni 10 pamoja na heshima ya kitaifa katika sekta ya fasihi.
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari Aprili 8, 2026, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda, amesema hafla ya utoaji tuzo itafanyika Aprili 13, 2026 katika Ukumbi wa Super Dome, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kuenzi kumbukumbu ya Baba wa Taifa, Julius Nyerere.
Amesema tuzo hiyo inayoratibiwa na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) imeendelea kuvutia washiriki wengi kutoka kada mbalimbali wakiwemo waandishi wa habari, walimu, wanafunzi na Watanzania waishio nje ya nchi, huku mwaka huu pia washiriki kutoka Jamhuri ya Czech wakijitokeza.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya Tuzo, Penina Mlama, majaji wamekamilisha uchambuzi wa miswada na tayari orodha ya washiriki bora katika nyanja nne—riwaya, ushairi, hadithi za watoto na tamthilia—imetolewa, huku washindi wakitarajiwa kutangazwa siku ya kilele cha tuzo.

Mbali na ushindani, hafla hiyo itatanguliwa na mjadala wa kitaaluma utakaowakutanisha wadau wa fasihi kutoka ndani na nje ya nchi, ambapo mshairi nguli Abdilatif Abdallah anatarajiwa kuwa mgeni rasmi. SOMA: ‘Kuna haja kuibua, kulea waandishi bunifu Watanzania’
Tangu kuanzishwa kwake, tuzo hiyo imeshawanufaisha waandishi 27, huku Serikali ikitumia zaidi ya Sh milioni 800 kuchapisha na kusambaza vitabu vilivyoshinda katika shule na maktaba, hatua inayolenga kukuza utamaduni wa kusoma na kuimarisha sekta ya uchapishaji nchini.