Wiki moja baada ya uchaguzi wa urais nchini Uganda, ambao rais aliye madarakani Yoweri Museveni alishinda kwa kishindo, kiongozi wa upinzani Bobi Wine anafutilia mbali matokeo. Katika mahojiano na RFI, anadai kuwa yuko mafichoni, anazungumzia hali ya ukandamizaji, na anasema ana ushahidi wa udanganyifu. Anatoa wito wa maandamano yasio na vurugu na kutoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuchukuwa hatua.

Imechapishwa: Imehaririwa:

Dakika 4 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Bobi Wine amefanya mahojiano na Christina Okello, mwenzetu wa kitengo cha RFI afrique.

RFI: Habari yako? Na zaidi ya yote: unahisi uko salama?

Bobi Wine: Niko hai… Ninapaswa kushukuru kuona bado nina pumua kufikia sasa. Lakini kuhusu usalama wangu: hapana, siko salama. Ninawindwa na jeshi wakati sijafanya uhalifu wowote. Niko mafichoni. Mke wangu na familia yangu hawako salama pia: wamezingirwa na jeshi. Hawawezi kuondoka, hakuna anayeweza kuingia. Wana njaa, na hata chakula wanachopelekewa kinakataliwa.

RFI: Tangu uchaguzi wa Januari 15, unaweza kuelezeaje hali ya sasa nchini Uganda?

Raia wetu wanauawa kwa kupigwa risasi. Kuna mauaji ya kimya kimya yanayoendelea. Mtoto wa Museveni alijitokeza siku mbili zilizopita na kusikitishwa kuona aliua “watu 22 pekee” kati ya wafausi wetu: angependa kuua zaidi. Pia tuna ripoti za watu zaidi ya 100 waliouawa kote nchini. Watu wanakamatwa wakati hawajafanya uhalifu wowote. Watu miongoni mwa manaibu wangu  wamekamatwa. Wawili kati yao ni wanawake, na sijui wako wapi. Walikamatwa siku moja kabla ya uchaguzi, na sasa zimepita siku saba: hakuna anayejua wako wapi. Naibu wangu anayesimamia eneo la kati pia alikamatwa leo (Alhamisi). Na hii inakuja baada ya kile kilichotokea wiki moja iliyopita, wakati watu kumi walipigwa risasi na kufariki ndani ya nyumba yake.

RFI: Unamaanisha mbunge wako, Muhammad Muwanga Kivumbi, kutoka wilaya ya Butambala. Anadai kwamba wafuasi wako kumi waliuawa siku ya uchaguzi, nyumbani kwake. Kwa upande wake, Rais Yoweri Museveni anawaita “magaidi,” akilenga NUP baada ya tukio hili. Unajibuje shutuma hizi, na unaamini nini kilitokea siku hiyo?

Kati ya watu hao kumi, wanane walikuwa wanawake. Jukumu lao lilikuwa kujaza fomu, kupokea matokeo, na kukusanya fomu za matangazo ya matokeo—“DR forms”—zilizowasilishwa kutoka vituo tofauti vya kupigia kura. Walikuwa nyumbani kwa mwanasiasa siku ya uchaguzi, na hapo ndipo polisi waliwakuta na kisha wakawaua kwa kuwapiga risasi.

RFI: Unalaani udanganyifu: una ushahidi gani halisi?

Tuna ushahidi wa kabla, wakati, na baada ya uchaguzi. Tuna video zinazoonyesha maafisa wa polisi, wanajeshi, na hata maafisa wa Tume ya Uchaguzi wakijaza kadi za kupigia kura kwa kumpendelea Yoweri Museveni. Tunazo nyingi kati ya hizo. Na licha ya hili, tulimshinda Museveni kwa tofauti kubwa. Kwa hivyo yeye na Tume waliamua kutosoma matokeo yoyote kutoka kwa fomu za tamko: walitengeneza asilimia na takwimu na kuzitangaza bila ushahidi. Tuliwaomba kuchapisha fomu hizi wilaya kwa wilaya: hawakufanya hivyo, kwa sababu wanajua hawana ushahidi huo.

RFI: Je, mtachukua hatua za kisheria kupinga matokeo?

Hapana. Hatuna imani na mfumo wa haki nchini Uganda: una upendeleo kwa Yoweri Museveni. Wafungwa wa kisiasa hawapatiwi dhamana. Na hata Mahakama Kuu inapotoa maamuzi, jeshi hupuuzia mbali. Kwa hivyo matumaini yetu hayako mahakamani: matumaini yetu yako kwa raia wa Uganda, wasimame na kukatae upuuzi huu wote.

RFI: Unapanga kufanya nini sasa? Mkakati wako ni upi? Na je, watu wafikirie kuwa utawania tena mwaka wa 2031?

Tunatoa wito kwa raia kutotii sheria. Tunatoa wito wa hatua zisizo za vurugu, maandamano yasiyo ya vurugu dhidi ya utawala, na aina zote za ubunifu za maandamano, hadi utawala utakapohisi shinikizo la raia. Hatuangalii hata mwaka wa 2031, au hata mwaka ujao: tunaangalia haraka iwezekanavyo kinachotakiwa kufanyika, kwa sababu utawala uliowekwa si chaguo letu. Lazima tujikomboe na kurejesha demokrasia.

RFI: Neno kwa wasikilizaji wetu kutoka nchi za Afrika zinazozungumza Kifaransa, hasa katika nchi ambazo upinzani pia unalaani tawala za kimabavu: ungependa kuwaambia nini?

Watu wanaoishi chini ya utawala wa kiimla kwingineko barani Afrika lazima waangalie kinachoendelea Uganda, kwa sababu tunateseka vivyo hivyo. Tunaweza kujifunza kutoka kwa kila mmoja na kusaidiana kwa kupaza zaidi sauti zetu.

RFI: Na unatarajia nini kutoka kwa jumuiya ya kimataifa?

Ninatoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuiwajibisha serikali ya Uganda. Pia nataka kuwashukuru: tunathamini—hata kama ni kwa kiwango kidogo—kinachofanywa kuunga mkono demokrasia na haki za binadamu barani Afrika. Lakini maadili yanayotuunganisha—demokrasia, haki za binadamu, utawala wa sheria—lazima yatumike kila mahali. Kiwango cha demokrasia barani Afrika kinapaswa kuwa sawa na Ulaya au Amerika Kusini. Kuwashtumu madikteta kama Lukashenko huko Belarus au Maduro huko Venezuela, huku madikteta barani Afrika wakipongezwa na kuwapa ushirikiano, ni ubaguzi wa rangi tu. Tunataka kutendewa kwa kiwango kile kile: wakati huduma ya intaneti inazimwa wakati wa uchaguzi, wakati raia wanauawa, na bado viongozi wa jumuiya ya kimataifa wanaendelea kushirikiana na madikteta wa Afrika kana kwamba wako halali, haikubaliki. Marekebisho kamili yanahitajika ili tuchukuliwe kuwa washirika wa kweli, kwa usawa.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *